Ofisi ya Taifa ya ukaguzi wa Hesabu za Serikali, (NAOT) imeanza mafunzo ya wiki moja kwa wakaguzi wake wapatao  120 yanayofanyika katika hoteli ya Giraffe Jijijni Dar es Salaam yenye lengo la kuwajengea uwezo  ili  kuwasaidia wakaguzi hao katika kazi zao za kila siku za ukaguzi.

“Ofisi yetu ni miongoni mwa Taasisi zinazoongoza katika kuwajengea uwezo wafanyakazi wake kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali ya ndani na nje ya nchi. Wadau na Serikali  yetu kwa ujumla wamekuwa makini katika kuhakikisha kwamba kwa pamoja tunapata mafunzo na kutimiza majukumu ya   kikatiba”

Hayo  yamesemwa  na Kaimu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu Bwana Francis Mwakapalila, wakati akifungua mafunzo  ya wiki moja  ambayo yameanza leo tarehe 21, Oktoba  na kutegemea kumalizika tarehe 25, Oktoba, 2013 huku  akiwataka wakaguzi hao kusoma  kwa makini na kuzingatia wanayofundishwa.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo , Mkurugenzi wa Rasilimali watu wa NAOT  Mama Salome Mollel, pia  amewataka wakaguzi hao kusoma kwa bidii  kwa sababu  lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo na kuongeza ufanisi katika kazi  zao za kila siku za ukaguzi.

Mafunzo hayo yanayotolewa na wakufunzi kutoka Ofisi ya Ukaguzi ya India,  yana lengo la kuwajengea uwezo wakaguzi hao kwa upande wa  ukaguzi wa mapato, ukaguzi wa  IT, na  Ukaguzi wa Umma  jinsi gani wataifanya  kazi yao kwa umakini zaidi na kupata matokeo mazuri zaidi wakati wa ukaguzi wanaoufanya kila wakati.